MASHAKA
Wajifanya umeganda, na mke wako wa ndani
Mwajifanya pete, chanda, heti wako abadani
Sasa ile misambwanda, unaitizama nini?
NJE KUNA MAMBO MENGI, LAZIMA TU REFRESH
MSHAMU
Sikiliza ndugu kaka, tamaa zitakuuwa
Jina lako tu Mashaka, maisha hujayajuwa
Tofauti naitaka, wapi unapochagua
KWANINI UNACHEPUKA?, WAKATI NI ILE ILE?
MASHAKA
Sio ile ile moja, Mkubwa una wehuka
mbona waleta viroja, ajabu kubwa ya mwaka
Nje napata faraja, NDANI gubu likiwaka
NJE KUNA MAMBO MENGI, LAZIMA TU REFRESH
MSHAMU
Gubu unajitakia, tabiazo si nzuri
Mke atakuwakia, unapoleta kiburi
Hatoweza vumilia, nje kwenda kuvinjari
KWANINI UNACHEPUKA?, WAKATI NI ILE ILE?
MASHAKA
hwenda weye una dhiki, ndo mana waleta hoja
MWANAUME haridhiki, na mwanamke mmoja
Mambo yako yakitiki, tutajakuwa pamoja
NJE KUNA MAMBO MENGI, LAZIMA TU REFRESH
MSHAMU
Mimi ni mume rijali, sikiliza wewe boya
Pande zote ni kamili, usinelewe vibaya
Nimeridhika na hali, sipendi hizo hekaya
KWANINI UNACHEPUKA, WAKATI NI ILE ILE
MASHAKA
Haya wewe tulizana, kwangu haiwezekani
Omba na mamie wana, asije anza uhuni
Tusije kutafutana, na kushikana ugoni
NJE KUNA MAMBO MENGI, LAZIMA TU REFRESH
MSHAMU
Ishike adabu yako, mwana izaya wahedi
Ubaki huko uliko, mwache wangu Mama Medi
Wanaokupa ujiko, Subiri na mijeledi
MWISHO WAKO NI MARADHI, NA ADHABU YA KABURI
MTUNZI
Kama una mushkeli, wewe utaniambia
Hawa vijana wawili, nani amekuvutia
Ni nani msema kweli, kwa ulivo jionea
@bunduki.com
COMMENTS